LANGUAGE :
English | Swahili

Sisi ni nani

 

Sikika ni shirika lisilo la kiserika lilililosajiliwa nchini Tanzania kwa lengo la kufanya ushawishi na utetezi juu ya utawala bora katika sekta ya afya. Shirika lilianzishwa mwaka 1999 likijulikana kama Youth Action Volunteers (YAV), na baadaye lilikua na kubadilika kutoka katika utetezi wa  afya ya uzazi kwa vijana na kujikita kwenye maeneo makuu ya msingi katika  sekta ya afya ambayo ni: Utawala na Usimamizi wa Fedha za Afya, Rasilimali Watu katika Afya, Madawa na Vifaa tiba pamoja na UKIMWI na Virusi vya UKIMWI.

 

Kwa sasa, tumeimarisha shughuli zetu katika maeneo ya vijijini ambayo ni Kondoa na Mpwapwa (Dodoma), Kiteto na Simanjiro (Manyara), Iramba na SingidaVijijini (Singida) ili kukukuza na kuimarisha  juhudi zilizokuwa zinatekelezwa awali mijini na kwenye miji midogo ikijumuisha  wilaya za Dar es Salaam na Kibaha

 

Tumeendelea kufanya utafiti mbalimbali wa kisayansi na kutumia matokeo na shuhuda za tafiti hizo kufanya utetezi katika ngazi zote za utoaji wa huduma za afya. Tunaendeleza utamaduni wetu wa kufanyakazi kwa kujitolea  na tunao wanajamii 70 wanaojitolea.  Vilevile tunatambua wananchi wote kama watumia huduma za afya. Hivyo basi, tunawezesha wanajamii wenyewe kushiriki  kikamilifu  katika Kusimamia Uwajibikaji na Kutathmini utoaji wa huduma za afya katika ngazi zote (SAM).

 

Sikika inatumia mbinu ya kupima matokeo ya kazi zake (Outcome Mapping) ili kutathmini mchango wa shughuli  hizo katika mabadiliko ya sekta ya afya nchini. Nguvu kubwa ya shughuli zetu za utetezi inatokana na  ubora wa utafiti tunaofanya pamoja na ushirikiano wa karibu na wadau na asasi zingine za kiraia.

Dira

Huduma bora za afya kwa watanzania wote.

 

Dhamira

Sikika inafanyakazi kuhakikisha usawa na upatikanaji wa huduma bora za afya kwa kutathmini mifumo ya afya na uwajibikaji katika ngazi zote za serikali.

 

Malengo

Sikika imedhamiria kufanikisha malengo makuu ya fuatayo:

  • Kukuza ufanisi katika bajeti ya sekta ya afya, uwazi na uwajibikaji katika ngazi zote za Serikali kuu na Serikali za Mitaa

  • Kuongeza kasma inayotengwa, mgawanyo wenye uwiano wa watumishi wa afya na uzingatiaji wa maadili ya taaluma ya afya

  • Kuongeza uwepo na upatikanaji,wa dawa na vifaa tiba katika ngazi zote za utoaji wa huduma za afya

  • Kukuza uwajibikaji katika usimamizi wa rasilimali za shughuli za UKIMWI katika ngazi zote za Serikali kuu na Mitaa

 

Shughuli zetu

Sikika inatekeleza shughuli zake katika maeneo makuu manne ya sekta ya afya ambayo ni: Utawala na Usimamizi wa Fedha za Afya, Rasilimali Watu katika Afya, Madawa na Vifaa tiba na UKIMWI naVirusi vya UKIMWI.

 

Utawala na Usimamizi wa Fedha za Afya

Idara ya Utawala na Usimamizi wa Fedha za Afyainafanyakazi kufikia malengo makuu matatu; kuongeza ufanisi wa bajeti,uwazi na uwajibikaji katika Serikali kuu pamoja na Serikali za mitaa. Katika kufanikisha malengo hayo,tunafanyakazi kwa karibu na wadau wakuu ambao ni Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii, Ofisi ya Waziri Mkuu-Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) na Kamati ya Bunge ya Huduma za Jamii ili kuchangia kuleta mabadiliko na kufikia malengo yaliyoorodheshwa.

Uwazi katika bajeti utakuza ushiriki wa wananchi kwenye mchakato mzima wa uandaaji wa bajeti na hivyo kuweka umiliki wa mchakato huo mikononi mwa wananchi. Kukuza ufanisi katika mgawanyo na matumizi ya rasilimali ndani ya sekta ya afya pamoja na usimamizi mzuri,utaboresha utoaji wahuduma za afya kwa wananchi wote.

 

Rasilimali Watu

Idara hii inalenga kuona ongezeko la bajeti ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa Rasilimali watu ndani ya sekta ya afya, mgawanyo sawa wa wafanyakazi na kuhakikisha watumishi wa afya wanafuata maadili na weledi wa taalumayao. Idara pia inafanya utafiti kuhusu usawa wa jinsia kwa kuzingatia Rasilimali Watu katika Afya na Fedha,  mafunzo, usajili waw afanyakazi,  mgawanyo, kudumu kazini na maadili ya kazi. Pia idara inaendesha mikutano na mijadala ya kujenga uwezo wa watumiaji na watoa huduma za afya kwenye ngazi ya Serikali za Mitaa na wabunge kwa lengo la kuboresha mfumo wa utoaji na upatikanaji wa huduma za afya nchini.

 

Dawa na Vifaa tiba

Idara hii inalenga kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba muhimu na vilivyo na ubora katika ngazi zote za utoaji wa huduma za afya nchini. Nguvu kubwa katika kufikia lengo hili imeelekezwa kwenye kuchochea uboreshaji wa mipango na bajeti za dawa na vifaa tiba pamoja na kuwezesha ushiriki wa wananchi katika ununuzi na usambazaji wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya huduma za afya vya umma.

Ili kuhakikisha kwamba malengo haya yanafikiwa, idara hii hufanya utafiti ili kupata picha ya hali halisi ya uwepo na upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika vituo vya huduma za afya vya umma. Lengo ni kufanya utetezi na kuboresha ufanisi huduma za Bohari Kuu ya Dawa ya taifa (MSD).

VVU/UKIMWI

Idara ya VVU/Ukimwi inafanyakazi kuhakikisha kuna upatikanaji wa huduma bora za afya kwa watu wanaoishi navirusi vya ukimwi (WAVIU). Kazi zinahusisha upatikanaji wa dawa za kupunguza makali ya virusi vya Ukimwi (ARVs), na upatikanaji wa dawa na vifaa tiba kama vile mashine za CD4.

 

Idara pia inafanyakazi kuhakikisha ufanisi unakuwepo katika mipango, mgawanyo wa bajeti na utekelezaji wa shughuli za VVU/Ukimwi kwa kuchambua mipango ya Serikali na wadau wa maendeleo na kuibua matumizi mabaya ya rasilimali, kuhamasisha kamati za VVU/Ukimwi ili ziweze kufanyakazi kwa ufanisi na kuwawezesha wananchi kudai haki zao.

 

Habari  na Mawasiliano

Idara hii ni kiunganishi muhimu kwa mawasiliano ya shirika. Ina jukumu la kukuza na kuimarisha  mawasiliano ya ndani na nje ya Sikika, kutangaza kazi za shirika na kuandaa mikakati ya kupashana  habari na utetezi miongoni mwa wadau, pamoja na kupata mrejesho kutoka kwao.

 

Usimamizi na Tathmini

Takriban miaka 10 iliyopita, tulikuwa tukifanya kazi kwa kutumia Jedwali la Mantiki, (Logical Framework) katika kusimamia na kutathmini kazi zetu. Wakati wa kufanya mapitio ya mkakati wetu tulifanya pia tathmini ya kina ya kazi zetu. Katika mchakato huo, tulijifunza kwamba mfumo wa jedwali la mantiki haukidhi matakwa yetu kwani haukutoa fursa ya kupima mchakato wa matokeo au mabadiliko yatokanayo na kazi zetu na kutambua mchango wa wadau wengine katika kufanikisha malengo yetu, jambo ambalo ni muhimu katika kazi ya utetezi endelevu. Hivyo basi, kuanzia 2011, Sikika ilianza rasmi kufuata mfumo wa kupima matokeo Outcome Mapping (OM) kama sehemu ya kufanya Usimamizi na Tathmini ya kazi zake (M&E).

 

Mfumo huu mpya unatoa nafasi ya kupanga kwa pamoja, kujadili na kutafakari shughuli tulizokubaliana kwa pamoja na washirika wetu. Washirika wetu ni wadau wote ambao wanaguswa moja kwa moja na mabadiliko tunayotarajia kutokana na kazi zetu. Mfumo huu unaruhusu kufanya mabadiliko ama marekebisho ya shughuli na mikakati  muda wowote katika kipindi  cha utekelezaji, kutokana na mrejesho na tunachojifunza kutoka kwa washirika wetu.  Mfumo huu pia umewezesha Sikika kujikita zaidi kwenye kupima matokeo kwa kuangalia mchango utokanao na kazi zetu na wakati huohuo kutambua mchango wa wadau wengine.